Thursday 10 July 2014

Rais-azindua-jengo-la-halmashauri-la-bil-2/-

samexa.blogsport.comjakaya-Mrisho-Kikwete_2d87f.jpg   RAIS Jakaya Kikwete jana amezindua Jengo la ofisi za Halmashauri ya wilaya ya Kilindi lililogharimu zaidi ya Sh bilioni mbili hadi kukamilika kwake.
Akisoma taarifa ya utekelezaji wa mradi huo kwa Rais Kikwete, Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya hiyo, Daudi Mayeji alisema jengo hilo la kisasa lina jumla ya vyumba 82 vya ofisi ikiwemo ukumbi mdogo na mkubwa.
Mayeji alisema mradi wa ujenzi wa jengo hilo la makao makuu ya Halmashauri ya wilaya hiyo ulianza rasmi mwaka 2007 baada ya serikali kutoa fedha za ujenzi.
Ujenzi ulifanywa na kampuni ya Mkandarasi AFRIQ Engeering and Construction Co. Limited, chini ya Mhandisi Mshauri National Estate Development Company Ltd (NEDCO).
Alisema katika mradi huo halmashauri hiyo ililazimika kuingia mikataba ya ujenzi wa jengo hilo kwa awamu mbili kutegemeana na upatikanaji wa fedha.
Wakati huo huo, katika kukabiliana na tatizo la maji katika kata ya Kwediboma iliyopo wilayani Kilindi serikali imetenga Sh bilioni 2.8 kwa ajili ya kukamilisha mradi wa maji safi kwenye vijiji kumi vinavyounda kata hiyo.
Rais Kikwete amebainisha hayo jana wakati akihutubia wananchi wa kata ya Kwediboma kabla ya kuzindua ujenzi wa mradi wa maji ya bomba wa kijiji cha Kwediboma unaotekelezwa kupitia mpango wa kuendeleza sekta ya maji kwa ufadhili wa Benki ya Dunia kwa kushirikiana na serikali ya Tanzania.
Alisema fedha hizo zimetengwa katika bajeti ya mwaka wa fedha ujao wa 2014/2015 kusaidia kupunguza ukubwa wa tatizo la upatikanaji wa huduma hiyo kwa wananchi hasa waishio maeneo ya vijijini.
“Ndugu zangu pamoja na serikali kuwekeza fedha hizi tambueni kwamba kama jamii mnalo jukumu kubwa la kuhakikisha mradi huu unatunzwa ili uwe endelevu kwa ajili ya kutoa huduma kwenu na vizazi vijavyo...naomba wananchi waote washiriki kutimiza jukumu hili ili kutoa huduma endelevu”, alisema Rais.
Vijiji vitakavyonufaika na huduma ya maji kupitia fedha hizo ni Mpalahala, Kwedigole, Kileguru, Mzinga ambavyo kwa sasa havina huduma ya maji hasa baada ya ya chanzo chao tegemezi ambacho kilikuwa ni Malambo mawili yaliyojengwa na halmashauri kupitia mradi wa DADPS kubomolewa na mvua msimu uliopita.
Awali akisoma taarifa kuhusu mradi huo, Katibu wa Kamati ya Mradi huo Ibrahimu Abdallah alisema hadi kukamilika kwake, unatarajiwa kugharimu Sh 517,364,391 na kwamba mpaka sasa zimetumika Sh 316,197,327 kwa ajili ya kukamilisha kazi za awamu ya kwanza ya mradi.
CHANZO:HABARILEO

Tuma Maoni 0718192930,E-mail samexavery@yahoo.com

No comments:

Post a Comment