Thursday 10 July 2014

Maoni-itafutwe-dawa-ya-utoro-baraza-la-wawakilishi.


Ssamexa.blogsport.com 
Kirusi cha utoro ambacho kimekuwa kikilitesa Bunge la Muungano wa Tanzania kwa muda mrefu, sasa kimeingia kwa kishindo kwenye Baraza la Wawakilishi (BLW), ambako shughuli za baraza hilo zimekuwa zikikwama kutokana na wajumbe kutohudhuria vikao. Hali hiyo ilijitokeza tena tangu wakati wa kikao cha kujadili bajeti ya mwaka wa fedha 2014/15 kilichoanza Mei 14, mwaka huu na kumalizika wiki iliyopi.            
Tatizo hilo la utoro wa wawakilishi wa wananchi hapa nchini awali lilidhaniwa kwamba ni la Bunge la Muungano pekee, ambako chombo hicho kwa miaka nenda miaka rudi kimekuwa kikikaa na kupitisha bajeti za Serikali na kufanya uamuzi katika mambo nyeti ya taifa pasipo kuwapo akidi, kinyume cha Katiba na Kanuni za Bunge. Udhaifu huo umekuwa tatizo sugu, kwani hata Bunge la Bajeti lililokaa mjini Dodoma kuanzia mwanzoni mwa Mei kujadili Bajeti ya mwaka 2014/15 lilimalizika wiki iliyopita likiwa limepitisha baadhi ya mambo nyeti pasipo kuwapo akidi.
Pamoja na utoro wa wabunge kwenye Bunge la Muungano kuwa tatizo sugu kiasi cha wananchi na wabunge wenyewe kuliona la kawaida, limekuwa halipigiwi kelele hata pale picha za magazeti na televisheni zinapoonyesha viti vingi bungeni vikiwa vitupu wakati vikao vya maamuzi muhimu vikiendelea. Tatizo hapa ni kukosekana vifungu katika Katiba au Kanuni za Bunge za kuwapa wananchi madaraka ya kuwawajibisha wawakilishi wao kwa kuwapigia kura ya kutokuwa na imani nao.
Hata hivyo, haikutazamiwa kwamba Baraza la Wawakilishi nalo lingekumbwa na tatizo hilo, kwani lilikuwa na mwenendo mzuri wa uwajibikaji baada ya kuanzishwa mwaka 1984 na kuendelea hivyo hadi mfumo wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK) ulipoanza baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010. Inasikitisha kwamba utoro sasa umeanza kuwa tatizo kubwa kwenye Baraza hilo, hata kuwaweka katika hali ngumu Spika Pandu Ameir Kificho, naibu wake, Ali Abdallah Ali na mwenyekiti wa Baraza hilo, Mgeni Hassan Juma kiasi cha chombo hicho kushindwa kukaa kama Kamati ya Matumizi kutokana na kutotimia akidi ya asilimia 50.
Katika tukio la wiki iliyopita, Naibu Spika Ali Abdallah Ali aliahirisha Baraza hilo kutokana na uchache wa wajumbe wakati wa kujadili bajeti ya Wizara ya Ardhi, Makazi, Maji na Nishati iliyowasilishwa na Waziri Ramadhan Abdallah Shaaban. Hivyo, Baraza hilo lisingeweza kukaa kama Kamati ya Matumizi na kupitisha vifungu kutokana na akidi ya wajumbe kutofikia asilimia 50. Tukio hilo lilitanguliwa na lile la Baraza hilo kushindwa kukaa kama Kamati ya Matumizi chini ya mwenyekiti wake, Mgeni Hassan Juma wakati wa kujadili bajeti ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Masoko. Hiyo ni mbali na matukio mawili ya awali, wakati Spika Kificho alipoliahirisha kwa sababu ya kukosekana akidi.
Tungependa kutoa hadhari kwa wajumbe wote wa BLW kwamba vitendo vyao vya utoro siyo tu ni utovu wa nidhamu, bali pia vinahatarisha uhai wao katika Baraza hilo.
Tofauti na wapigakura wa Tanzania Bara, wenzao wa Zanzibar ni makini mno katika kufuatilia uwajibikaji wa wawakilishi wao, kwani historia imeonyesha kuwa, pamoja na kutokubali kuhongwa, hawana simile wala huruma na wawakilishi wanaowasaliti kwa kutotimiza wajibu wao.
CHANZO:MWANANACHI

Tuma Maoni 0718192930,E-mail samexavery@yahoo.com

No comments:

Post a Comment